Tuesday, April 12, 2011

HADITHI

Palikuwa na kijiji cha Mtunguchoya ,kata ya Legezamwendo,tarafa ya Madongokuinama,jamii ya zeruzeru, palikuwa na mzee mmoja aitwae mzee Toboamambo.Mzee Toboamambo alikuwa na watoto wawili Tototundu na Chongo.Mzee Toboamambo alichukiwa sana pale kijijini kwao kutokana na tabia yake ya kutoa taarifa kwa uongozi wa kijiji na vyombo vya dora kwa kila ovu aliloliona pale kijijini.

Viongozi wa halmashauri ya kijiji walimpenda sana mzee huyu kutokana na ushirikiano wake,Alikuwa mpenda maendeleo asiyeogopa kupigania maendeleo ya kijiji chake.Katika kijiji kile palikuwa na msitu mkubwa ulijulikana kwa jina la Takalang’onyo.Msitu huu ulikuwa mkubwa mno wenye vyannzo vya maji na kila rasilimali inayo patikana katika misitu.Msitu ulikuwa wakijani na ulitunzwa vizuri kutokana na mahitaji ya kimila ya jamii ya zeruzeru.Waliutumia msitu huu kwa kufanya shughuli za kimila kamavile matambiko,ibada za jadi na kwa mahitaji ya nyumbani kama vile kuni,kuchimba dawa za asili na matunda.Katika msitu ule kulikuwa na chanzo cha maji kikubwa ambacho kilitoa maji kwa kata nzima ya Legezamwendo.

Jamii ya zeruzeru iliuvamia ule msitu na kuchunga mifugo,waliuza miti ya mbao na kuchoma mkaa.Mwishoe msitu ulitoweka na chanzo cha maji kilikauka. Kulitokea mafunzo ya uhamasishaji wa utunzaji wa mazingira yaliyoongozwa na shirika la watu wa marekani.Mzee Toboamambo alibahatika kuteuliwa na uongoziwa kijiji cha Mtunguchoya kushiriki katika mafunzo hayo.Mafunzo yalihusu ushirikishwaji wa jamii katika maswala ya uhifadhi wa misitu.

Baada ya mafunzo hayo, Mzee Toboamambo aliomba kuusimamia msitu wa Takalang’onyo ili ausimamie.Uongozi wa halmashauri ya kijiji cha Mtunguchoya ulimkabidhi Mzee Toboamambo ule msitu.Baada ya kukabidhiwa msitu Mzee Toboamambo alitafuta bunduki na kutoa tangazo kwamba ,haruhusiwi mtu yeyote kukanyaga katika eneo la msitu wa takalang’onyo wala mifugo ya aina yeyote ile.Ilipotokea ngo’ombe au mbuzi au punda alipoingia msituni alishambuliwa na bunduki na kufa.Upande mwingine aliwaweka wanae kumsaidia katika shughuli ya ulinzi.Tototundu alitumia manati-nyundo kuua kuku na bata walioingia msituni.Chongo aliyekuwa na jicho moja, alikaa juu ya mti mrefu kuliangaza jicho lake pande zote za msitu kuona ni nani anaingia msituni.Pindi alipoona mtu au kitu chochote kifugwacho na binadamu kinaingia msituni alitoa taarifa kwa baba na mdogo wakeTototundu.

Yapata miaka kumi kupita baada ya mzee Toboamambo kuulinda msitu wa Takalang’onyo.Msitu ulistawi vizuri sana,vyanzo vya maji vilitiririsha maji na mvua ilinyesha kwa msimu uliotakiwa.

Kutokana na mfumo alioutumia Mzee Toboamambo kuhifadhi msitu wa Takalang’onyo,jamii nzima ya zeruzeru ilimchukia kupindukia.Hiyo wana jamii waliitana kujadili jinsi ya kupambana na Mzee Toboamambo kulingana na mauaji ambayo mzee huyu alishayafanya. Wanajamii walimvamia mzee huyu na kumuua kwa kumkatakata na mapanga katika vipande vidogodogo pamoja na wanawe wote wawili.
Baada ya kumua mzee Toboamambo jamii ya zeruzeru iliuvamia msitu wa takalang’onyo na kuushambulia kwa kukata miti ya mbao, kuchoma mkaa, kuchunga mifugo, na kuuchoma moto mara kwa mara na hatimaye msitu wa takalang’onyo ulitoweka.Vyanzo vya maji vilikauka,mvua ilianza kunyesha mara mojamoja na hatimaye maisha yalibadilikakabisa.Uchumi wa wanajamii ya zeruzeru ulianza kudidimia na maisha yakawa magumu.Watu walianza kulalamika kuwa Mungu amewaacha na mwishoe walikumbwa na matatizo anuawai na inchi ikawa kame.

FUNDISHO
Jamii ina kila haki ya kushirikishwa na kupewa elimu juu ya utekelezaji wa mradi wowote wenye manufaa kwa jamii husika.Katika hadithi tumeona kwamba uongozi wa halmashauri ya kijiji cha mtunguchoya haukushirikisha jamii katika swala zima la uhifadhi wa mazingira ndio maana kulitokea mgogoro kati ya mzee Toboamambo na wanakijiji cha Mtunguchoya.Jamii ikihusishwa katika shughuli za maendeleo na kushiriki kikamilifu,kijiji hicho kitakuwa na maendeleo ya kudumu.
YETs tusiende kwenye jamii zetu na tukawa na fikra za mzee Toboamambo. Hatunabudi kuonesha kuwa sisi ni mawakara wa mabadiliko katika swala zima la mazingira.
Prepared by;
Anselmo Wami-YET 2011

No comments:

Post a Comment